Wasiliana nasi | FAQ | Mails | Malalamiko |

Tanga Regional Referral Hospital
(Bombo Hospital)

WATAKIWA KUWA NA UTAMADUNI WA KUFANYA UCHUNGUZI WA AFYA YA KINYWA NA MENO MARA KWA MARA

Posted on: February 11th, 2024






Na Oscar Assenga, TANGA.

DAKTARI Mwandamizi wa Magonjwa ya Kinywa na Meno katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga, Dkt Onesmo Ezekiel amewashauri wananchi wa mkoa huo kuwa na utamaduni wa kufanya uchunguzi wa kinywa na meno mara bili kwa mwaka ili kuepukana na magonjwa mbalimbali yanayoweza kukutana nayo ikiwemo ya kung’oa jino

Dkt Onesmo ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Kinywa na Meno Katika Hospitali hiyo aliyasema hayo leo wakati akizungumza na mtandao huo ambapo alisema uchunguzi huo wanaweza kufanya bila hata kuumwa kwa sababu magonjwa ya kinywa na meno katika hatua za awali hayana dalili zozote.

Alisema ila dalili zinaanza kujitokeza wakati ugonjwa unakuwa tayari upo kwenye hatua za mbele zaidi hivyo unapokwenda daktari ukiwa na maumivu na kukuangalia kama kuna uwezekano wa kuzuia magonjwa ya kinywa na meno unakuta tayari umeshaathiri eneo kubwa na hivyo kuwa na uchaguzi mmoja wa kung’oa jino.

“Lakini niwaambie kwamba dalili za meno ukiziwahi kwenye hatua za awali inakuwa rahisi kufanya matibabu na gharama zake zinakuwa ni rahisi vyenginevyo utakwenda kwa daktari ukiwa na maumivu makubwa zaidi na hivyo kuwa na uchaguzi wa kungo’a jino”Alisema

Hata hivyo Dkt Onesmo alisema kwamba magonjwa hayo yanaathiri watoto na watu wazima hivyo kuwataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wanazingatia suala la usafi wa kinywa na meno vizuri wasimamiwe watumie dawa ya mswaki yenye madini ya floride,calcium na karafuu .

“Lakini mswaki wanaoutumia usizidi zaidi ya miezi mitatu kwa sababu baada ya miezi hiyo unashindwa kufanya kazi zake kwa ufanisi huku asisisitiza umuhimu wa jamii kuhakikisha wanatunza vinywa vyao kwa kuzingatia kufanya usafi mara kwa mara”Alisema

Akizungumza kuhusu kitengo cha huduma ya Afya ya Kinywa na Meno katika Hospitali hiyo Dkt Onesmo alisema wanatoa huduma zinazohusiana na magonjwa ya kinywa na meno kila siku za Jumatatu hadi Ijumaa kuanzia saa mbili na nusu mpaka saa tisa na nusu mchana.

“Pia wakati mwengine tunatoa huduma siku za wikiendi linapokuwa limejitokeza suala la uhitaji na kitengo chetu kina vitengo kadhaa ndani yake ambapo tunatoa huduma za meno bandia,kuziba meno,kusafisha meno,kufanya matibabu ya mzizi wa jino na kungarisha jino “Alisema

Alisema pia wakati mwengine wanalazimika kwenda chumba cha upasuaji inatpokea kuna mahitaji mfano wanapotokea wagonjwa wenye uvimbe ambao unahitaji kufanyiwa upasuaji mkubwa au wagonjwa wa ajali ambao matibabu yao ili kuweza kuwatibu wanapaswa kwenda chumba cha upasuaji.

“Tunafanya upasuaji mdogo ambao hauhitaji mgonjwa kulazwa bali isipokuwa ikiwekewa ganzi katika eneo husika anaweza kufanyiwa huduma hizo na kuruhusiwa“Alisema.

Hata hivyo alisema kwamba hospitali hiyo inapokea inapokea wagonjwa kutoka wilaya zote za mkoa huo na wanapata matibabu hapo na wachache wanalazimika kuwapa rufaa kwendfa kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Akizungumzia magonjwa yanayowatesa wananchi wengi,Dkt Onesmo alisema magonjwa hayo ni kutoboka kwa meno ambao zaidi ya nusu ya wagonjwa ni tatizo kubwa na wengine ni fizi kutoka damu na yamekuwa yakiathiri watu wa umri zote.

“Kuanzia vijana,watoto hadi wazee wa jinsia zote wanakaribiana huku kundi jingine ni wale wanaopata ajali za kuvunjika taya la chini na la juu au yote mawili pamoja au kung’oka meno kwa ajili ya ajali ambazo zinahusisha bodaboda ambao wamekuwa wamelewa”Alisema